UANDISHI WA INSHA
Uandishi ni kitendo cha kupangilia maneno katika maandishi. Mada hii inazungumzia uandishi wa insha za wasifu kwa umahususi wake. Kabla ya kuanza uandishi utajifunza mambo muhimu yanayopaswa kuzingatiwa katika uandishi wa insha kwa ujumla. Utaelewa muundo wa insha na mwisho utajifunza juu ya dhana ya insha ya wasifu na namna inavyoandikwa na mwisho kabisa utaangalia mfano wa insha ya wasifu.
Insha ya wasifu ni ile ya kutoa maelezo juu ya jinsi mtu au kitu kilivyo, tabia, vitendo na mandhari (sura ya mahali jinsi panavyoonekana).
Mambo muhimu katika insha ya wasifu ni: sura, rangi, umbo, vipimo, tabia, na kadhalika. Insha hizi zinaweza kuongelea kitu chochote kile, inaweza kuwa ni mnyama, mtu, Shule, nchi na kadhalika.
Hatua za Uandishi wa Insha
Elezea hatua za uandishi wa insha
Kabla ya kuanza kuandika insha, ni muhimu sana uamue unataka kuandika juu ya nini. Inafaa uchague ile mada iliyo rahisi kwako kuweza kujieleza kikamilifu na kwa urahisi.
Kama unaandika insha za kufanyia mazoezi ni heri uchague mada zenye habari ambazo unazielewa. Iwapo hulijui au hulielewi jambo, ufanye uchunguzi kwanza. Ukisha kupata habari muhimu ndipo baadaye uandike insha yako kulingana na jinsi unavyoijua na jinsi unavyoikumbuka habari inayohusika.
Katika mtihani ni muhimu uyasome maagizo kwa makini. Kwa mfano, maagizo yanaweza kuwa: Chagua mojawapo ya habari zifuatazo kisha uandike insha isiyopungua kurasa mbili za karatasi za majibu.
Au:
Chagua mojawapo ya habari hizi kisha uandike insha ya maneno yasiyopungua 400.
Ni heri uandike insha nzuri ya kiwango kinachotakiwa kuliko ndefu (zaidi ya maneno 400) ambayo haitakuwa na mambo muhimu hadi mwisho, na pengine yenye makosa na uchafu mwingi kupindukia. Ni muhimu ikumbukwe jinsi insha ilivyo ndefu, hasa katika mtihani, ndivyo idadi ya makosa inavyozidi kuongezeka.
Muundo wa Insha
Fafanua muundo wa insha
Katika uandishi wa insha, muundo wake unakuwa na vitu vifuatavyo:
  1. Kichwa cha insha; kichwa cha insha hudokeza kile ulichokijadili katika insha yako. Kwa mfano: Madhara ya matumizi ya madawa ya kulevya n.k
  2. Utangulizi; Mambo yaliyopo katika utangulizi ni pamoja na kutoa fasili ya maneno muhimu na kuelezea kwa muhtasari mambo ambayo utakwenda kuyajadili katika insha yako.
  3. Kiini cha insha; katika kiini ndipo kuna maelezo ya kina juu ya kile unachokijadili katika insha yako, maelezo haya yanakuwa katika aya kadhaa kulingana na idadi ya hoja ulizonazo katika mjadala wako.
  4. Hitimisho; hapa ndipo kuna muhtasari wa kile kilichojadiliwa katika kiini cha insha au inaweza kuwa ni msimamo juu ya kile kilichohadiliwa katika insha.
Hebu soma mfano ufuatao wa insha ya wasifu:
Example 1
SHULE YANGU
Shule yangu inaitwa Shule ya Sekondari ya Mwananchi. Ni shule ya zamani iliyoanzishwa siku ya Ijumaa, tarehe 5 Agosti 1966 na Mheshimiwa Donna Matembele, aliyekuwa diwani wa kata ya Masuba.
Shule hii ambayo ni maarufu sana ipo katika Tarafa ya Mkunazini. Imejengwa katika uwanja wa hekta kumi na mbili. Ina madarasa kumi na mawili ya vidato vinne vya mikondo mitatu kila kimoja. Ina wanafunzi mia tano na wanne badala ya idadi halali ya wanafunzi mia nne themanini. Ni shule inayopendwa sana.
Wanafunzi wa kike ni mia mbili na watatu na wa kiume ni mia tatu na mmoja. Walimu ni thelathini na mmoja. Jamii hii inapendana sana. Wanafunzi wana imani kubwa sana na walimu wao. Walimu huwahimiza wawe wanafanya bidii katika kazi na masomo kwa ujumla.
Wanafunzi hukadiria ugumu wa mazoezi wapewayo. Yale wayaonayo kuwa ni rahisi wao hujifanyia. Yale magumu kidogo hushughulikia kwa pamoja kwa kusaidiana wenyewe kwa wenyewe. Walimu hushirikishwa tu wakati wa mazoezi tata.
Shule ya Sekondari ya Mwananchi ni ya kuvutia sana. Ina miti mingi sana ya matunda. Ina maua ya aina aina. Kutokana na nidhamu na uwajibikaji matunda hukomaa ndipo yatumiwe kwa mpango wakati wa chakula.
Heshima imethaminiwa mno na wanafunzi. Wanaheshimiana na kuwaheshimu walimu wao. Kwao heshima ni utiifu na uzingativu. Kutii na kuzingatia mambo waambiwayo na walimu ndicho kipimo cha heshima.
Katika shule yangu wanafunzi tuko kama paka. Paka hamtumi mtu nyama lakini atunukiwapo kipande hawezi kumruhusu yeyote kukigusa. Nasi tutunukiwapo nafasi yoyote ya kusoma hatumruhusu mtu yeyote kutupokonya nafasi hiyo.
Wanafunzi wa shule wana sare zao za kuvutia wazivaazo kiungwana kabisa. Sare hizo ni sweta ya bluu, shati au blauzi ya samawati, tai ya rangi ya damu ya mzee, suruali ndefu au sketi ya kijani kibichi, viatu vyeusi vya soli ndogo na visigino vifupi.
Katika shule yetu kuna uhusianao mwema baina ya walimu, wazazi, Chama cha Wazazi na Walimu (CHAWAWA) na Baraza la Shule. Kamati ya CHAWAWA na Baraza la Shule huanzisha miradi na kuitekeleza haraka kutokana na wazazi kuiunga mkono.
Kwa muda mrefu sasa matokeo ya mitihani yamekuwa ya kuridhisha kabisa. Na si hayo peke yake. Wanafunzi washirikipo katika michezo ya mpira, ya riadha na matamasha ya muziki takribani mara zote huibuka washindi.
Kwa ufupi shule yangu ni ya mafanikio mengi.
Mambo muhimu ya kuzingtiwa katika insha hii ya wasifu:
  • KICHWA (Shule yangu).
  • MAELEZO KAMILI yenye:
  • JINA la shule
  • HISTORIA ya shule
  • MAZINGIRA ya shule
  • IDADI ya wanafunzi na walimu
  • HALI ya wanafunzi
  • MAFANIKIO ya shule.
  • HITIMISHO lenye sifa ya jumla.
Insha za Kisanaa na zisizo za Kisanaa
Tofautisha insha za kisanaa na zisizo za kisanaa
Activity 1
Tofautisha insha za kisanaa na zisizo za kisanaa

logoblog

No comments:

Post a Comment